Breaking News

EMEDO NA TMA WAZINDUA MFUMO MPYA WA UTOAJI WA TAARIFA ZA HALI YA HEWA KWA WAVUVI

 Na Tonny Alphonce,Goziba

Katika juhudi za kuhakikisha usalama wa Wavuvi na Wadau wa uvuvi katika Ziwa Victoria, Shirika la Usimamizi wa Mazingira na Maendeleo (EMEDO), kwa kushirikiana na Mamlaka ya Utabiri wa Hali ya Hewa (TMA) Kanda ya Ziwa, wamezindua mfumo mpya wa utoaji wa taarifa za hali ya hewa kwa jamii ya wavuvi wa Kisiwa cha Goziba.

Uzinduzi huo umefanyika tarehe 1 Oktoba 2024, na kuhudhuriwa na wavuvi, wamiliki wa mitumbwi, wafanyabiashara wa samaki, na viongozi wa serikali.

Mfumo huu wa utoaji wa taarifa za hali ya hewa unategemea mabango maalumu yatakayotumika kuonesha hali ya hewa kwa urahisi, ili wavuvi na wadau wa shughuli za uvuvi waweze kupata taarifa kwa wakati na kuelewa hali ya hewa kabla ya kuingia ziwani.

Hatua hii inakuja baada ya utafiti uliofanywa na EMEDO mwaka 2021, ambao ulibaini kuwa moja ya sababu za ajali za mara kwa mara za kuzama kwa wavuvi ni upungufu wa taarifa za utabiri wa hali ya hewa kwa wakati sahihi na uelewa wa taarifa hizo.

Utafiti wa EMEDO ulionyesha kuwa wavuvi wengi wamekuwa wakikosa taarifa sahihi za hali ya hewa, hali inayosababisha ajali za kuzama na kupoteza maisha kwa baadhi yao. Ili kutatua changamoto hiyo, EMEDO kwa kushirikiana na TMA wameanzisha mfumo huu wa mabango.

Wananchi wa kisiwa cha Goziba wakielekezwa namna gani mabango yatakavyokuwa yakitoa taarifa ya hali ya hewa kwa wakazi wa kisiwa hicho.

Kwanza, mabango haya yamewekwa katika Kisiwa cha Goziba, na yanatarajiwa kusaidia sana katika kupunguza ajali za majini kwa kuwapa wavuvi taarifa za utabiri wa hali ya hewa kwa urahisi.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mabango hayo, Meneja wa TMA Kanda ya Ziwa, Augustino Nduganda, alielezea umuhimu wa mfumo huo kwa wavuvi na wadau wote wa uvuvi. 

Meneja wa TMA Kanda ya Ziwa, Augustino Nduganda akiongea na wananchi wa Goziba.
Alisisitiza kuwa kupata taarifa sahihi za hali ya hewa ni muhimu kwa maisha na mali zao.

Meneja wa TMA Kanda ya Ziwa, Augustino Nduganda akielezea namna taarifa za hali ya hewa zitakavyokuwa zikiwekwa kwenye mabango ya taarifa.

"Tumefikia hatua hii kutokana na utafiti uliofanywa na wenzetu wa EMEDO. Tulikaa chini tukajiuliza mfumo gani ungekuwa rahisi na bora kwa wavuvi, na tukapata jawabu la mabango haya. Kwa picha tu, mnaweza kujua hali ya hewa ikoje kwa siku hiyo," alisema Nduganda.

Nduganda aliongeza kuwa taarifa za hali ya hewa zitakuwa zinatolewa mara mbili kwa siku. Saa sita mchana kwa ajili ya wafanyabiashara wa samaki, na saa tisa alasiri kwa wavuvi wanaoelekea ziwani usiku.

Arthur Mgema, Meneja wa Mradi wa Kuzuia Ajali za Kuzama kwa Wavuvi kutoka EMEDO, alitoa wito kwa wavuvi wa Kisiwa cha Goziba kutumia mabango haya kabla ya kuingia ziwani.

Arthur Mugema, Meneja wa Mradi wa Kuzuia Ajali za Kuzama kwa Wavuvi kutoka EMEDO akizungumzia umuhimu wa mabango ya taarifa ya hali ya hewa yaliyowekwa katika kisiwa cha Goziba.

Alisema kuwa mfumo huo umekuwa ni matokeo ya jitihada za muda mrefu za kutatua changamoto zinazosababisha ajali kwa wavuvi.

"Kupitia mradi huu wa kuzuia kuzama maji, tumekuwa tukitatua changamoto moja baada ya nyingine tukiongozwa na utafiti wetu wa mwaka 2021.

Taarifa sahihi za hali ya hewa ni jambo ambalo wavuvi walikuwa wanahitaji sana, na sasa limefanyiwa kazi," alisema Mgema.

Arthur Mugema, Meneja wa Mradi wa Kuzuia Ajali za Kuzama kwa Wavuvi kutoka EMEDO akizungumzia umuhimu wa kuvaa Life Jacket wakati wakiwa majini.

Utafiti uliofanywa na Shirika la EMEDO mwaka 2021 ulibaini sababu mbalimbali zinazopelekea Wavuvi kuzama maji na wengine kupoteza maisha na sababu moja wapo ilibainika kuwa ni changamoto ya upatikana wa taarifa za utabiri wa hali ya hewa kwa wakati na uelewa kuhusu taarifa zenyewe na ili kutatua changamoto hiyo EMEDO na TMA wamefanikiwa kuja na mabango yatakayotoa taarifa za hali ya hewa kwa jamii ya wavuvi na kwa kuanza wameanza na kisiwa cha Goziba.


No comments