Breaking News

NSSF YACHANGAMKIA FURSA YA UTOAJI ELIMU YA HIFADHI YA JAMII TAMASHA LA KIZIMKAZI 2024

    

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), Bw. Masha Mshomba, amesema Maonesho ya Tamasha la Kizimkazi 2024 kwa upande wa NSSF ni fursa kwa sababu yanakutanisha watu kutoka maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi, hivyo Mfuko unapata fursa ya kutoa elimu ya hifadhi ya jamii kutoka sekta binafsi na sekta isiyo rasmi pamoja na kuangalia fursa mbalimbali ikiwa ni pamoja na uwekezaji.

Bw. Mshomba amesema hayo tarehe 20 Agosti, 2024 mara baada ya kufungwa kwa mafunzo ya Tamasha la Kizimkazi 2024, yaliyofanyika katika Uwanja wa Mwehe, Makunduchi Mkoa wa Kusini Unguja, tarehe 20 Agosti, 2024. Katika hafla hiyo mgeni rasmi alikuwa Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, ambapo Mfuko ulitoa hundi ya shilingi milioni 50 kwa ajili ya kuunga mkono shughuli za kilimo biashara.

Amesema NSSF  inatumia fursa ya uwepo wa matamasha kama la Kizimkazi kwa sababu ina jukumu la kuifikia sekta rasmi na sekta isiyo rasmi ambayo imebeba kundi kubwa likiwemo la wakulima, wavuvi, wafugaji na wajasiriamali wengine.

Bw. Mshomba amewahakikishia Watanzania kuwa, NSSF imedhamira kuwafikia wajasiriamali waliopo maeneo mbalimbali nchini, ili kuwapatia elimu ya hifadhi ya jamii na kujiunga na Mfuko.

"Nazidi kuwahakikishia Watanzania kuwa NSSF tuna dhamira ya dhati ya kuwafikia vijana hususan wajasiriamali nchini nzima na kuwapa elimu ya hifadhi ya jamii, kuwaandikisha ili waweze kujiwekea akiba kwa maisha yao ya sasa na ya baadaye," amesema Bw. Mshomba.

Amesema NSSF itaendelea kufikisha elimu ya hifadhi ya jamii kwa makundi mbalimbali yaliyopo katika sekta binafsi na sekta isiyo kwani hiyo ndio azma ya msingi ya kuandikisha Watanzania wengi ili wanufaike na sekta ya hifadhi.
   

No comments