Breaking News

MTOTO ANATAKIWA KULINDWA NA KUONYESHWA UPENDO TANGU AKIWA TUMBONI

 Na Tonny Alphonce,Mwanza

Kina mama wajawazito na jamii kwa jumla wametakiwa kuwekeza zaidi kipindi cha ujauzito kwa kuwa katika kipindi hicho mama amebeba mtoto ambaye anatakiwa kuanza kujengewa misingi ya maisha kuanzia akiwa na mwaka sifuri.

Sister  Denise Mattle akizungumza katika warsha ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto iliyoandaliwa na Montessori Hubb.

Kauli hiyo imetolewa na Sister  Denise Mattle katika warsha ya malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto iliyoandaliwa na Montessori Hubb ikiwa na lengo la kujadili mambo mtambuka yanayohusu malezi,makuzi na maendeleo ya awali ya mtoto pamoja na chngamoto za malezi katika zama hizi za utandawazi.

Akiwasilisha mada ya malezi sister Denise amesema bado kuna makosa mengi yanayofanywa na walezi kuanzia mama anapokuwa mjamzito ambapo familia nyingine huanza kumshambulia mama kwa maneno makali ambayo humuumiza mama na mtoto kwa ujumla.

“Mtoto akiwa tumboni huwasiliana na mama kupitia neva kwa maana hiyo mama akiwa na huzuni na mtoto pia hupata huzuni na hata baada ya kuzaliwa kama baba au mama akiwa mkali kwa mtoto basi mtoto huathirika moja kwa moja na ndio maana tunawataka wazazi wajitahidi kuongea na watoto kwa lugha rafiki kwa kuwa mtoto katika umri wa 0-6 au 0 – 7 hujifunza kwa kusikia au kushika na akihitaji kitu huanza kulia kama ishara ya kuomba”.alisema Sister Denise.

Sister Denise amesema matokeo ya mtoto aliyelelewa kimakosa hupata matatizo ya kisaikolojia ambapo  huanza kuonekana pale anapoanza shule ambapo mtoto huonekana muoga,hawezi kujieleza,hajiamini kwa kuwa katika kipindi cha ukuaji wake wa ubongo na kimwili aliingiziwa vitu hivyo ambapo humuathiri hadi katika utu uzima wake.

Kwa upande wake Matesha Sembuche akizungumzia Elimu ya Awali ya Montessori amesema wao katika hatua za ujifunzaji za awali za mtoto wanafundisha watoto kwa vitendo kwa kutumia vifaa ambavyo huviona nyumbani ambapo humjenga katika kuanza kuandika na kusoma.

Matesha Sembuche akizungumza na wazazi na walezi juu ya  Elimu ya Awali ya Montessori jinsi ilivyotofauti na shule zingine.

"Watoto tunawapa maumbo ya vitu mbalimbali,tunawapa chupa za maji wafungue,tunawapa chupa ya chai wafungue pamoja na mambo mengine na kila kitendo huwa na maana kubwa kwa kwa mtoto kwa mfano kufungua chupa mtoto anatumia vidole vitatu ambavyo atakuja kuvitumia katika kuandika kwa maana hiyo wale ambao husema ooh Montessori watoto hawasomi wanacheza tu wanakosea sana".alisema Matesha.

Amesema kupitia vifaa walivyonavyo vyenyewe vimelenga kuimarisha milango mitano ya fahamu ya mtoto ili kuanzia mapema mtoto aweze kutofautisha mambo ikiwemo harufu,ladha na mambo mengine ambayo huamuliwa na milango ya fahamu.

Naye afisa ustawi wa jamii kutoka wilaya ya Ilemela Pamela Javi amewataka walimu na wazazi kushirikiana katika malezi ya mtoto ili kumlinda mtoto na vitendo vya kikatili ambavyo vinaweza kufanywa nyumbani au shuleni.


Afisa Ustawi wa Jamii kutoka wilaya ya Ilemela Pamela Javi akiwasilisha mada juu ya Ulinzi na Usalama wa mtoto.

"Wazazi na walimu naomba niwaambie utafiti uliofanywa na UNICEF unaonyesha asilimia 60 ya vitendo vya kikatili kwa mtoto hufanyika nyumbani na asilimia 40 ya vitendo vya kikatili pia hufanyika shuleni kwa maana hiyo sisi wote hapa lazima tutafakari tujue namna gani tutamlinda mtoto popote anapokuwa"s.alisema Pamela

Pamela amesema mtoto anapofanyiwa ukatili humsababishia maumivu ya muda mfupi na muda mrefu na ndio maana kuna watoto walifanyiwa ukatili utotoni na wao baada ya kukua wanatafuta namna ya kulipiza walichofanyiwa na hivyo kusababisha vitendo vya kikatili kuendelea kutokea katika jamii.

Michael Sungusia meneja miradi kutoka Montessori akizungumzia lengo la kuanzishwa kwa Montessori Hubb.

Michael Sungusia meneja miradi kutoka Montessori amesema kwa miaka 26 sasa Montessori Community of Tanzania imekuwa ikiendesha mbinu za  ya ufundishaji na ujifunzaji kwa kusaidia ukuaji  wa mtoto kwa manufaa ya taifa na kwa hivi sasa wanaungana na serikali katika kutekeleza  Program Jumuishi  ya Malezi,Makuzi na Maendeleo ya wali ya mtoto kwa kuweka katika uhimizaji  na ukuzaji wa malezi jumuishi yenye tija kwa taifa kwa kuzingatia  vipengele vya Afya bora ,Lishe tosherevu,Ulizi na Usalama ,Malezi yenye mwitikio chanya pamoja na Fursa za ujifunzaji wa awali.

No comments