Breaking News

ILEMELA YAOMBA WADAU KUSAIDIA KUTOKOMEZA VITENDO VYA UKATILI KWA WATOTO

 Na Tonny Alphonce,Mwanza

Mkuu wa wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza Hassan Masala amewataka wadau wanaofanyakazi na kundi la wanawake na Watoto mkoani Mwanza kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha vitendo vya ukatili vikiwemo vya unyanyasaji watoto kijinsia vinakomeshwa.


Mkuu wa wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza Hassan Masala akizungumza na wadau wa kupambana na vitendo vya ukatili kwa wanawake na watoto.

Akizungumza katika kikao cha kujadili hali ya vitendo vya ukatili kwa wilaya ya Ilemela kilichoandaliwa na shirika la Wadada Solution Mh Masala amesema ofisi yake imekuwa ikipokea taarifa mbalimbali kutoka mitaani ambapo kuna Watoto wameripotiwa kubakwa pamoja na matukio ya mimba za utotoni.

‘Twendeni tushirikiane kuibua matendo yanayofanyika mtaani kwetu,twendeni tuendelee kupaza sauti kwa waathirika kwa sababu kuna hata wazazi wanaficha matendo wanaofanyiwa Watoto sasa haya yote yanatakiwa kuwekwa wazi ili serikali ijue namna ya kupambana na vitendo hivi’.alisema Masala.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa shirika la Wadada Solution Lucy John amesema wameendelea kutoa elimu mbalimbali za namna ya kukomesha vitendo vya kikatili kama ambavyo wameweza kutoa elimu hiyo kwa wadau mbalimbali wanaogusa makundi ya wanawake na Watoto.

Mkurugenzi wa shirika la Wadada Solution Lucy John 

Lucy amesema kikao hicho ni muhimu kwa kuwa wadau hawa wamekuwa wakisahaulika katika kukumbushwa juu ya matendo haya ya ukatili kama ambavyo elimu hutolewa katika makundi mengine.

‘Pengo ambalo tumeliona ni ukosefu wa elimu katika familia nyingi kuhusu suala zima la malezi na ndio maana vitendo vingine vingi vinatokea katika familia zetu na kwa sasa kazi kubwa tunayoifanya ni kutoa elimu hii’.alisema Lucy.

Elihaika Josphat ambae ni afisa mradi wa mradi wa kijana paza sauti chukua hatua amesema katika kuhakikisha taifa linakuwa na wazazi wanaojitambua wamekuwa wakitoa elimu ya uzazi katika kata za wilaya ya Ilemela ambazo ni Sangabuye,Shibula,Bugogwa na Kitangili.

Elihaika ameitaka jamii kuripoti matendo yote ya kikatili katika ngazi mbalimbali zikiwemo za nyumbani na hata mashuleni ambako vitendo hivi vimeripotiwa kufanyika kwa wingi.

Wakati wilaya ya Ilemela ikiwaomba wadau kusaidia kufichua vitendo vya ukatili dhidi ya Watoto inaelezwa kuwa kuna upungufu wa utoaji taarifa za kesi za unyanyasaji na utelekezaji wa Watoto kuanzia umri 0 – 8.

Kuna utafiti mdogo ulifanywa kwenye jamii  kuhusiana na kesi za ukatili ,unyanyasaji,utelekezaji na unyanyasaji wa Watoto  wadogo uliofanywa na wazazi na walezi.

Baadhi ya wadau walioshiriki kikao cha kujadiliana kuhusu hali ya ukatili kwa wanawake na watoto.

Utafiti uliofanywa na Benki ya Dunia katika mkoa wa Katavi ulionyesha asilimia 18 ya wazazi wenye Watoto chini ya miaka mitatu huwapiga vibao Watoto wao hali kadhalika asilimia 5 ya wazazi walionekana wakiwapiga vibao wakati wa utafiti wenyewe.

Ripoti ya shirika la kimataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) inayohusiana na ukatili dhidi ya watoto Tanzania inaonyesha kuwa msichana 1 kti ya 3 na Mvulana 1 kati ya 3 wanapitia aina mbalimbalin za ukatili kingono kabla hawajafikisha miaka 18.

No comments